Machapisho

Mke akimwangalia mume wake mwenye ugonjwa wa akili


 HABARI KUU

Mambo Unayopaswa Kujua Kuhusu Magonjwa ya Akili

“Nilihisi kana kwamba pumzi zimeniishia,” anasema Claudia, ambaye alikuwa ametoka tu kuambiwa kwamba anaugua ugonjwa wa kubadilika-badilika kwa hisia na ugonjwa wa mfadhaiko unaosababishwa na tukio lenye kutisha. “Ilikuwa vigumu sana kukabiliana na hali hiyo ngumu.”

Mark, mume wa Claudia anasema, “Ilituchukua muda mrefu kukubali hali hiyo. Hata hivyo nilitambua kwamba ninapaswa kuendelea kumfariji mke wangu.”

IKIWA wewe au mtu unayempenda angegunduliwa kuwa ana ugonjwa fulani wa akili, ungehisije? Jambo zuri ni kwamba ugonjwa wa akili unaweza kutibiwa. Acheni tuchunguze mambo fulani yanayoweza kutusaidia kuyaelewa vizuri magonjwa ya akili. *

 Taarifa Muhimu Kuhusu Magonjwa ya Akili

“Mamilioni ya watu kotekote duniani wana magonjwa ya akili na jambo hilo huwaathiri sana wapendwa wao. Inasemekana kwamba mmoja kati ya watu wanne ataugua ugonjwa wa akili wakati fulani maishani. Ugonjwa wa kushuka moyo ndio kisababishi kikubwa cha magonjwa ya akili. Pia, ugonjwa wa Schizophrenia na ule wa kubadilika-badilika kwa hisia ni miongoni mwa magonjwa yanayowadhoofisha watu wengi. . . . Ingawa watu wengi leo wanaugua magonjwa ya akili, magonjwa hayo hupuuzwa na hayashughulikiwi sana au wagonjwa huaibikia hali yao.”—Shirika la Afya Ulimwenguni.

Kulingana na Shirika la Afya Ulimwenguni, watu wengi wanaougua magonjwa ya akili hawatafuti matibabu kwa sababu ya kuogopa jinsi jamii itakavyowaona.

Ripoti moja ya Shirika la Kitaifa la Magonjwa ya Akili nchini Marekani inasema kwamba ingawa magonjwa ya akili yana tiba, nchini humo takribani asilimia 60 ya watu wazima na karibia asilimia 50 ya vijana wenye umri wa kati ya miaka 8 hadi 15 wanaougua magonjwa ya akili hawakutibiwa katika mwaka uliopita.

 Kuyaelewa Magonjwa ya Akili

Mwanamke mwenye ugonjwa wa akili

Ugonjwa wa akili ni nini? Wataalamu wanafafanua ugonjwa wa akili kuwa tatizo kubwa la akili linaloathiri uwezo wa mtu wa kufikiri, kudhibiti hisia na tabia. Kwa kawaida hali hiyo huvuruga uwezo wa mtu wa kufurahia uhusiano mzuri na kukabiliana na changamoto za maisha.

Mtu hapatwi na ugonjwa wa akili kwa sababu ya udhaifu au tabia fulani aliyonayo

Athari za ugonjwa wa akili hutofautiana ikitegemea muda na kadiri ambayo mtu ameugua na pia, hali za mgonjwa na aina ya ugonjwa anaougua. Ugonjwa wa akili unaweza kumpata mwanamume au mwanamke, tajiri au maskini, na mtu wa umri wowote, tamaduni, jamii, dini, au kiwango chochote cha elimu. Mtu hapatwi na ugonjwa wa akili kwa sababu ya udhaifu au tabia fulani aliyo nayo. Mgonjwa akitibiwa vizuri, anaweza kupona na kuendelea kuishi maisha yake ya kawaida.

Kutibu Magonjwa ya Akili

Madaktari wanaweza kutibu magonjwa mengi ya akili. Basi, hatua ya kwanza muhimu ni kuchunguzwa na daktari stadi mwenye uzoefu wa kutibu magonjwa ya akili.

Mwanamke mwenye ugonjwa wa akili akizungumza na daktari

Hata hivyo, wale wanaougua magonjwa hayo wanaweza kunufaika iwapo tu watakubali kupokea tiba inayofaa. Hiyo inamaanisha kusema waziwazi kuhusu ugonjwa wa akili wanaougua. Matibabu hayo huenda yakatia ndani kuzungumza na madaktari wenye uzoefu ambao watamsaidia mgonjwa kuelewa hali yake, kusuluhisha matatizo ya kila siku, na kumsisitizia uhitaji wa kushikamana na utaratibu wa matibabu. Rafiki au mtu wa familia anaweza kuwa msaada mkubwa wakati wa mazungumzo hayo kwa kumfariji mgonjwa na kumpa utegemezo anaohitaji.

Watu wengi wamejua jinsi ya kushughulika na magonjwa ya akili baada ya kuelewa vizuri hali yao na kuzingatia utaratibu wa matibabu yaliyopendekezwa na madaktari. Mark aliyetajwa awali anasema hivi: “Kabla ya mke wangu kugunduliwa kuwa anaugua ugonjwa wa akili, hatukuelewa mambo mengi kuhusu magonjwa hayo. Lakini tumejifunza kushughulika na kila jambo hatua kwa hatua na kukabiliana na kila hali jinsi ilivyo. Kwa kipindi fulani sasa, tumefaidika kutokana na msaada ambao madaktari, marafiki na watu wa familia wametoa.”

Hatua ya kwanza muhimu ni kuchunguzwa vizuri na daktari mwenye uzoefu

 Claudia anakubaliana na jambo hilo. Anasema hivi: “Mwanzoni nilipogunduliwa kuwa nina ugonjwa wa akili nilijihisi kama mfungwa gerezani. Na ingawa tatizo hili linanizuia mimi na mume wangu tusifanye mengi, nimejifunza kwamba hata mambo yanayoonekana kuwa magumu yanaweza kutimizwa. Kwa hiyo ninakabiliana na tatizo langu kwa kufuata mashauri ninayopata kutoka kwa madaktari wanaonitibu, kusitawisha uhusiano mzuri na wengine, na kushughulikia jambo moja baada ya lingine.”

Afya ya Kiroho Ni Muhimu Sana

Mwanamke akisoma Biblia

Biblia haisemi kwamba mtu akiwa na afya ya kiroho basi matatizo yake ya afya ya kimwili yataisha. Hata hivyo, familia nyingi kote duniani zimefarijika na kuimarishwa na mafundisho ya Biblia. Kwa mfano, Biblia inatuhakikishia kwamba Muumba wetu mwenye upendo huwafariji wale “waliovunjika moyo” na “waliopondwa roho.” —Zaburi 34:18.

Ingawa Biblia si kitabu cha mambo ya afya, inatoa mwongozo stadi unaoweza kutusaidia tukabiliane na maumivu ya kihisia na hali zinazotutaabisha. Pia, Biblia inatupa tumaini la wakati ujao, wakati ambapo watu wote duniani wataishi bila magonjwa au uchungu wowote. Neno la Mungu linaahidi hivi: “Wakati huo macho ya vipofu yatafunguliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Wakati huo kilema atapanda juu kama vile paa anavyofanya, na ulimi wa bubu utapaaza sauti kwa furaha.”—Isaya 35:5, 6.